Wednesday, October 3, 2012

Tamko rasmi la HakiElimu juu ya Kampeni ya kuboresha Elimu ya Awali Nchini


Mkurugenzi wa HakiElimu Elizabeth Missokia atoa tamko siku ya uzinduzi wa kampeni ya kuboresha elimu ya awali.Pembeni ni Mratibu wa shirika la Tahea kutoka Mwanza Bi Mary Kabati.

Leo tarehe 27 Septemba  2012, shirika la  HakiElimu linazindua kampeni ambayo imepewa jina la “Boresha Elimu ya Chekechea”. Lengo la kampeni hii ni kuitaka Serikali itimize ahadi na wajibu wake wa kutoa elimu bora kwa wanafunzi wote wa elimu ya awali) ambayo ni muhimu sana katika kujenga msingi imara kielimu. Ni ukweli usiopingika  kuwaelimu ya awali itolewapo kikamilifu,  huwa ni msingi imara  kwa mtoto katika elimu yake ya baadae.
Elimu ya Awali ni muhimu kwa maendeleo ya mtoto kimwili, kiakili na kimaadili. Katika Sera ya Elimu na mafunzo ya mwaka 1995 Serikali inaonesha umuhimu wa elimu ya awali,inapotamka ; Tafiti kadhaa zilizofanyika nchini katika miaka ya 1980 zilibaini kuwa watoto waliopitia elimu ya awali huwa na mafanikio makubwa zaidi wanapoanza darasa la kwanza. Kutokana na kutambua umuhimu huu, Serikali iliamua kuingiza Elimu ya Awali kwa watoto wenye umri wa miaka 5 na 6 kwenye mfumo rasmi wa elimu na kila shule ya msingi inapaswa kuwa na madarasa ya Elimu ya Awali.”
Sera ya Elimu na Mafunzo 2010. Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi . Toleo jipya Rasimu ya 2 March 2011.(uk 5-6).

Uwekezaji katika huduma bora kwa mtoto na elimu ya awali huwa na faida maradufu kwa watoto wetu- ambao ni raia wetu wa  baadaye. Walipa kodi nao pia hufaidika na huimarisha uchumi. Faida ya uwekezaji wa fedha za umma katika elimu bora ya awali ni kubwa sana. Lakini je, Tanzania imeligundua hili na kulitekelezakikamilifu?  Na je, maneno haya ambayo sera inasisitiza yako yanatekelezwa kwa vitendo?

Baada ya kufanya tafiti katika sehemu mbalimbali nchini  HakiElimu inasikitishwa na jinsi ambavyo elimu ya awali inavyotolewa katika mazingira yasiyofaa hali inayochangia kushuka kwa kiwango cha elimu nchini.  Kama ilivyo katika elimu ya msingi na ile ya sekondari , elimu ya awali imegubikwa na changamoto nyingi. Baadhi ya changamoto hizi ni  upungufu mkubwa wa vyumba vya madarasa, unaosababisha mrundikano mkubwa katika madarasa,  ukosefu mkubwa wa walimu wenye taaluma ya elimu ya awali pamoja na vifaa vya kufundishia. Aidha, kutokuwepo na tofauti ya kimadarasa katika elimu ya awali ( yaani watoto wa umri wa miaka 5 na miaka 6 kusoma katika darasa moja), na wingi wa masomo pia ni changamoto. 
Baadhi ya wanafunzi wa awali kutoka shule ya msingi Mchangani kutoka Mwananyamala Dar es Salaam

Akiwasilisha Bungeni makadirio na matumizi ya wizara yake kwa mwaka 2012/2013, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi ,  Dkt Shukuru Kawambwa, alisema Serikali ilitoa mwongozo unaoelekeza kila shule ya Msingi kufanya Serikali imeelekeza  yafuatayo katika sekta ya elimu nchini kuhusiana na Elimu ya Awali:
(i)                 Kuhakisha kuwa kila shule ya msingi ina darasa la Elimu ya Awali, lenye madawati yanayolingana na hali ya watoto wa elimu hiyo,
(ii)               Kujenga vyoo kwa ajili ya watoto wa Elimu ya Awali wasiingiliane na wale wa shule za msingi.
(iii)             Kuandaa waalimu wengi wa Elimu ya Awali na kuwapanga katika shule zinazohusika
Katika kutekeleza maagizo hayo  Serikali ilitoa mwongozo unaoelekeza kila shule ya msingi kuwa na darasa la Elimu ya Awali. Pia wizara iliahidi kushirikiana na Halmashauri ili kuhakikisha kuwa Elimu ya Awali inapata rasilimali stahiki kama inavyoelekezwa katika MMEM II, ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa walimu na vifaa vya kufundishia na kujifunzia.

Lakini licha ya agizo hilo pamoja na makubaliano mengine yaliyofikiwa na serikali katika mwaka wa fedha 2012/2013, Serikali haijatenga kiasi chochote cha fedha kwa ajili ya elimu ya Awali. Hili linatupa wasiwasi wadau wa elimu kama kweli Serikali ina nia ya dhati  kuboresha elimu ya awali nchini au bado inaendelea kuja na mikakati ambayo haina utekelezaji.
Baada ya kuona madhara ya kukosa elimu bora ya awali kwa watoto wetu, HakiElimu inatoa wito kwa watanzania wote nchini wenye mapenzi mema na maendeleo ya taifa letu kuungana nasi katika kampeni hii kwa njia zifuatazo;
  • Kuhimiza wananchi wote wenye watoto wenye umri wa kuandikishwa shule za awali wafanye hivyo kwa wingi. Kuna baadhi ya sehemu inaripotiwa wazazi bado hawajaelewa umuhimu wa kuwapeleka watoto katika madarasa haya ya awali.
  •  Kuwabana viongozi wetu tuliowachagua kuanzia mwenyekiti wa mtaa, diwani na Wabunge wetuwanachukua hatua kukabiliana na changamoto zilizopo ili kufanikisha Elimu bora ya Awali kwa watoto wetu.
  • Wananchi kuandika barua kwenye magazeti mbalimbali hapa nchini zikielezea hali ya elimu ya awali inavyotolewa katika maeneo mliyopo. Barua hizo mnaweza kuzituma moja kwa moja kwenda kwa Wahariri wa  magazeti mnayoyasoma kupitia anuani zilizopo katika gazeti ulipendalo. Vilevile mnaweza kututumia barua hizo kupitia sanduku letu la barua 79401 DSM; zikiwa na kichwa cha habari ‘BORESHA CHEKECHEA’. Sisi tutazipeleka katika magazeti mbalimbali nchini na zitachapishwa na kufikisha ujumbe kwa viongozi wetu.
  • Aidha, ili kuchagiza mafanikio katika sekta hii ya elimu, HakiElimu imeandaa vipindi vya radio katika mikoa ya Morogoro, Mbeya, Tabora, Tanga, Kagera, Dodoma na Mara ambavyo vitatoa nafasi ya Marafiki wa Elimu kujadili jinsi gani elimu ya awali inaweza kuboreshwa hapa nchini na nini kifanyike. Katika vipindi hivyo vinavyoendeshwa na Marafiki wa Elimu wananchi wote mnaombwa kupiga simu na kutoa mchango wa nini kifanyike ili kuboresha elimu ya awali nchini.
  • Hali kadhalika, kwa watanzania wanaotumia mtandao wa Internet tunawaomba mshiriki kampeni hii kwa kutembelea mtandao wetu wa facebook katika www.facebook.com/hakielimu,mtandao wa twitter unaopatikana kupitia www.twitter.com/hakielimu na blog yetu inayopatikana kupitia  www.hakielimu.blogspot.com.
Sambamba na hilo, leo tarehe 27 Septemba, 2012, HakiElimu inazindua matangazo mawili ya radio na televisheni yatakayokuwa yakiruka katika vituo vya radio na televisheni takribani 12 nchini Tanzania.  Moja ya matangazo hayo litaonesha changamoto zilizoko katika elimu ya awali nchini na tangazo la pili litaonesha mfano wa shule bora au elimu ya awali tunayoitaka nchini Tanzania.  Tunaomba mtumie dakika zisizozidi 3 kuangalia matangazo ambayo pia yanapatikana katika mtandao wetu wa YouTube kupitia www.youtube.com/hakielimutz
Imetolewa na

Bi. Elizabeth Missokia
Mkurugenzi Mtendaji – HakiElimu
27 Septemba 2012

0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More