Friday, November 4, 2011

Shairi maalum: HakiElimu hongera kumuenzi Kambarage

Mkurugenzi wa HakiElimu Bi. Elizabeth Missokia

HakiElimu hongera kumuenzi Kambarage

Shairi na mwl Magali; Shule ya msingi Mwisenge

Karibu wageni wetu, shuleni kwetu Mwisenge,

Wageni wakuu wetu, karibuni tujiunge,

Furaha kuu ipo kwetu, wananchi msijitenge,

HakiElimu hongera, kumuenzi Kambarage.

Mradi huu wa Maktaba, jamii ilitamani,

HakiElimu ndiyo Mwamba, Maktaba kujengeni,

Njoo Mama nawe Baba, Watoto wahimizeni,

HakiElimu hongera, kumuenzi Kambarage.

Mashirika yapo mengi, lakini hili hawakuona,

na mikoa iko mingi, Mara wao waliona,

miradi wanayo mingi, shule ya JK kuiona,

HakiElimu hongera, kumuenzi Kambarage.

Kwenye vyombo vya habari, Twaziona kazi zenu,

Sasa tumewaona wazi, Maktaba ipo kwetu,

Imebaki moja kazi, kusoma bila uchovu,

HakiElimu hongera, kumuenzi kambarage.

Wanafunzi sote jamani, jitihada tuongezeni,

Tusome na tutunzeni, vitabu vitafuteni,

Tusizurure mitaani, taaluma tuinueni,

HakiElimu hongera, kumuenzi Kambarage.

Jografia kuelewa, vitabu kukisomeni,

Historia na mazingira, afya tutajueni,

Biashara na TEHAMA, HakiElimu asanteni,

HakiElimu hongera, kumuenzi Kambarage.

HakiElimu hongereni, kumuenzi Kambarage

Uhuru tusherekeeni, jitihada za Kambarage

Nyayo zake tufuateni, sifa katupa Mwisenge

HakiElimu hongera, kumuenzi Kambarage

Wanafunzi pia wazazi, Elimu ni mkombozi,

Lazima tuweni wazi, elimu itoe mzizi,

Utoro na huo wizi, hivyo havina nafasi,

HakiElimu hongera, kumuenzi Kambarage.

Leo tunawaahidini, kusoma pasipo kuchoka,

Masharti tufuateni, maktaba tumefaidika,

Leo twawatangazieni, Mwisenge tutasikika,

HakiElimu hongera kumuenzi Kambarage.

Hayatuishi mdomoni, HakiElimu na Mwisenge,

Asante twawalipeni, rudini tena Mwisenge,

Bado twawahitajini, michezo pia tucheze,

HakiElimu hongera, kumuenzi Kambarage



1 comments:

naitwa beatrice mollel, ninawapongeza haki elimu kwa kutimiza miaka 10 tangu kuanziswa. Vilevile ninawapongeza kwa kujali haki za watoto, nakujali masilai ya walimu wao.Kwa mfano kuangalia mapungufu yao na kuyasemea kwa njia mbalimbali,kama vile kurusha vipindi vinavyousu shida zao na haki sitahiki. hongereni sana kwa kazi nzito ya kutetea masilai ya watu wetu.

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More