Monday, November 28, 2011

Makwetta: Viongozi wababaishaji ndio chanzo cha kuporomoka kwa elimu nchini


Mwanaharakati ISLAM MPOSSO kulia akiwa na mhadhiri wa chuo kikuu Dr. Kitila Mkumbo kulia pamoja na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Shule Kuu ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano ya Umma, Ayub Rioba wakati wa kongamano la Miaka hamsini na tafakari ya sekta ya elimu Tanzania iliyofanyika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Na Islam Mposso

KUPOROMOKA kwa elimu nchini kunatokana na Tanzania kuwa na viongozi wababaishaji, wasemaji wa maneno mengi, wasiotekeleza wanayoyasema na kukosa ufuatiliaji.

Hayo yamo kwenye hotuba iliyopatikana kwa maandishi kutoka kwa Waziri wa Elimu wa serikali ya kwanza, Jackson Makwetta :Ilisomeka "Tanzania ni kama mama mjamzito ambaye siku zake za kujifungua zimefikia lakini, hajifungui.”

Hotuba hiyo ilikuwa kwaajili ya Kongamano la Kujadili Elimu na Mustakabali wake katika Miaka 50 ya Uhuru, lililoandaliwa na HakiElimu kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Alisema kuwa Tanzania inahitaji kufanyiwa mabadiliko vinginevyo itaendelea kudidimia kiuchumi.

Makwetta alilalamika kuwa: “Tatizo kubwa la nchi hii ni serikali kutofuatilia, wala si tatizo la kukosekana kwa sera. Hili ni taifa la wasemaji maneno na siyo taifa la watekelezaji." Alisema mapendekezo ya tume aliyoisimamia na kupewa jina ‘Makwetta’ ya mwaka 1982 mapendekezo yake yamewekwa kabatini hadi sasa, badala ya kufanyiwa kazi licha ya kukubaliwa na serikali.

“Hayatekelezwi kwa sababu wahusika hawataki kupata taabu,” ilisema wakati akitoa mada hiyo na kuongeza: “Sasa naelewa kwa nini V.I Lenin (Viladimir Illich Lenin mwasisi wa taifa la Urusi), alisema matumizi ya nguvu ni lazima kwa mama aliyefikia siku za kujifungua. Akitoa mada katika kongamano hilo naye Profesa Herme Mosha, alisema kuwa, tatizo la Tanzania ni viongozi wake kutofuata sera za elimu zilizopo.

Alisema kuwa wakati wa kusherehekea Miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania Bara yapo baadhi ya mambo ambayo watu wanapaswa kusema hapana, ikiwa ni pamoja na watoto kukaa chini madarasani, watoto kujazana madarasani na utekelezaji mbovu wa miradi na mipango ya elimu.

Naye Dk Kitila Mkumbo alisema kuwa, kwa sasa taifa lazima liamue kukubaliana na maoni ya wataalamu kuhusu lugha ya kufundishia kama iwe ni Kiswahili, hali aliyosema itawasaidia wanafunzi kuelewa vyema wanachofundishwa darasani.


0 comments:

Post a Comment

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More